Saturday 5 September 2015

Fahamu Namna ya Kushughulikia Matatizo la Tezi Dume (Prostate Disorders)

Illustration of normal prostate.
Tezi dume ni sehemu mojawapo ya mfumo wa uzazi wa kiume. Inaundwa na sehemu mbili, lobes, ambazo zimeunganishwa na kufunikwa kwa nje kwa utando wa tishu. Tezi hii ipo mbele kidogo ya puru (rectum) na kwenye shina la kibofu cha mkojo na mwanzo wa mrija wa mkojo (urethra). Tezi dume inauzunguka mrija unaounganisha kibofu cha mkojo na uume. Tezi dume ina upana wa takriban 3.8 cm, urefu 2.5cm na uzito takriban 25 grams.

Takriban theluthi moja (1/3) ya wanaume wote duniani waliovuka umri wa miaka 50 wana matatizo ya tezi dume. Hali hii huongezeka kufikia asilimia 75 kwa wanaume wenye umri wa miaka 80. Matatizo ya kuvimba kwa tezi na matatizo ya ufanyaji kazi wa kibofu cha mkojo (bladder disorders) huweza kusababisha magonjwa kama maumivu ya viungo vya mwili (arthritis), matatizo ya figo (kidney disorders) na uremia.

Tezi dume ni muhimu katika utoaji wa mkojo kwenye kibofu cha mkojo. Pia kazi za tezi dume ni kutoa majimaji yanayochanganyika na mbegu za kiume (sperms) wakati wa kilele cha tendo la ngono. Mchanganyiko huu wa mbegu pamoja na majimaji hayo hufanya shahawa (semen). Aidha majimaji hayo husaidia kuzipa mbegu za kiume nguvu ya kusafiri kwenye uke mpaka kufikia kwenye mirija ya fallopian tayari kwa utungisho na yai la kike. Vilevile husaidia kupunguza hali ya kitindikali iliyopo katika uke, ambayo kama isiporekebishwa, huweza kuua mbegu nyingi za kiume na kufanya utungisho kuwa wa tabu.

Kuvimba Tezi Dume (BPH)
Kwa kadiri mwanaume anavyozeeka, ni jambo la kawaida pia kwa tezi dume kuongezeka ukubwa na kuvimba. Hali hii kitabibu huitwa Benign Prostate Hyperplasia au wengine hupenda kutumia maneno Benign Prostate Hypertrophy kwa kifupi BPH.
Ukuaji wa tezi dume hupitia hatua kuu mbili. Hatua ya kwanza hutokea kipindi cha balehe wakati tezi dume linapoongezeka ukubwa na kuwa mara mbili ya lilivyokuwa hapo awali. Baada ya hapo ukuaji husimama kwa muda mpaka kijana anapofikisha miaka 25 hadi 30 ndipo hatua ya pili ya ukuaji huanza tena. Ukuaji huendelea kwa viwango na kasi tofauti kati ya mtu na mtu na hatimaye kusababisha BPH katika umri wa utu uzima.
Wakati tezi dume linapokua na kutanuka, utando wa tishu unaozulizunguka hutanuka pia. Hata hivyo ingawa tezi dume huendelea kukua, hufikia wakati utando wake huacha kutanuka na kufanya tezi dume kubana mrija wa kutolea mkojo kutoka kwenye kibofu. Hali hii husababisha kibofu cha mkojo kuwa na ngozi ngumu. Hali hii hufanya kibofu cha mkojo kuhisi kutaka kutoa mkojo nje hata kama kiasi cha mkojo ndani yake ni kidogo sana. Hufikia wakati, kibofu huwa dhaifu na kupoteza uwezo wake wa kuhisi kutoa mkojo na hivyo kufanya mtu anapokojoa kushindwa kutoa mkojo wote na badala yake hubakiza kiasi fulani cha mkojo kwenye kibofu.

BPH husababishwa na nini?
Chanzo halisi cha BPH au vihatarishi vyake (risk factors) havijulikani kwa uhakika. Kwa muda mrefu imekuwa ikichukuliwa kuwa BPH hutokea kwa wanaume watu wazima na wazee tu. Aidha imewahi kuonekana huko nyuma kuwa PBH haitokei kwa wanaume ambao wamewahi kufanyiwa operesheni ya kuondoa korodani au wale ambao walizaliwa bila korodani. Hali imepelekea baadhi ya watafiti kuamini kuwa BPH ina uhusiano mkubwa na umri wa mtu pamoja na uwepo wa korodani.
Kuna dhana (theories) kadhaa zinazojaribu kuelezea chanzo cha BPH. Dhana hizo ni pamoja na


1.     Uhusiano kati ya BPH na homoni ya estrogen: Wanaume huzalisha testosterone, homoni ya muhimu sana katika mwili wa mwanaume. Hali kadhalika huzalisha pia estrogen ambayo ni homoni ya kike kwa kiwango kidogo sana. Kadiri jinsi mtu anavyozeeka, ndivyo uzalishaji wa testosterone unavyokuwa mdogo na kufanya kiwango chake katika damu kupungua kulinganisha na kiwango cha estrogen ambacho huongezeka kwa kiasi fulani. Pamoja na kazi nyingine, estrogen pia huchochea ukuaji wa chembe hai za mwili. Tafiti zilizofanywa kwa wanyama zimeonesha kuwa BPH hutokea kwa sababu kiwango kikubwa cha estrogen katika damu huchochea ukuaji wa seli za tezi dume na hivyo kufanya tezi dume kuvimba.
2.     Uhusiano kati ya BPH na Dihydrotestosterone (DHT): DHT ni kiasili kinachozalishwa kutokana na testosterone kwenye tezi dume, ambacho husaidia kuthibiti ukuaji wa tezi dume. Ingawa wanyama wengi hupoteza uwezo wa kuzalisha DHT wanapofikia umri wa uzee, baadhi ya tafiti zimeonesha kuwa, kwa binadamu, hata kama kiwango cha testosterone kitapungua sana katika damu, wanaume watu wazima bado wana uwezo wa kuzalisha kiasili hiki cha DHT katika tezi dume zao. Uzalishaji na uklimbikaji huu wa DHT huchochea kwa kiasi kikubwa ukuaji wa seli za tezi dume na kusababisha BPH. Wanasayansi wamegundua kuwa wanaume watu wazima wenye kiwango kidogo cha DHT hawapati BPH.
3.     Uhusiano kati ya BPH na maelekezo ya seli: Dhana nyingine inasema kwamba baadhi ya seli kutoka katika sehemu fulani ya matezi yanayohusika na ukuaji mwilini hupewa maelekezo wakati mtu anapokuwa bado mdogo. Seli hizi hutunza maelekezo hayo na baada ya miaka kadhaa maelekezo haya huanzwa kutekelezwa na seli za matezi mengine. Mojawapo ya melekezo hayo ni kuchochea ukuaji wa tezi dume na kusababisha BPH.

Dalili za BPH
Dalili za BPH hutokea kwa sababu ya kubanwa kwa njia ya kutoa mkojo nje ya mwili (urethra) au kibofu kushindwa kuthibiti mkojo. Aidha dalili hizi hutofautiana kati ya mtu na mtu, ingawa karibu wagonjwa wote
 


1.     Hukojoa mkojo unaokatika katika
2.     Hukojoa mkojo wenye mtiririko dhaifu
3.     Husita kabla ya kuanza kukojoa
4.     Hali ya kujihisi kubanwa na mkojo kila mara
5.     Kushindwa kuthibiti mkojo kiasi cha mkojo kutirika wenyewe
6.     Hali ya kuhisi mkojo haujaisha kwenye kibofu
7.     hukojoa mara kwa mara hasa nyakati za usiku
8.     Kushindwa kukojoa kabisa (urine retention)
9.     Au dalili zinazotokana na madhara ya BPH

Madhara ya BPH
BPH kama ilivyo saratani ya tezi dume, inaweza kumletea mgonjwa madhara (complications) kadhaa. Madhara hayo ni pamoja na:
 

1.     Mkojo kushindwa kutoka (retention of urine)
2.     Mgandamizo kwenye kibofu cha mkojo
3.     Vijiwe kwenye kibofu cha mkojo
4.     Uambukizi katika njia ya mkojo (UTI)
5.     Madhara katika figo au kibofu
6.     Shinikizo la damu
7.     Kushindwa kutoa shahawa kwenye uume (retrograde ejaculation)
8.     Maambukizi mbalimbali
9.     Nimonia (Pneumonia)
10.   Damu kuganda
11.   Uhanithi

Vipimo na Uchunguzi

Baada ya mgonjwa kujihisi dalili zilizotajwa hapo juu, daktari atamfanyia uchunguzi wa mwili kabla ya kumfanyia vipimo zaidi. Vipimo vyaweza kutofautiana kati ya mgonjwa namgonjwa, lakini baadhi ya vipimo ni pamoja na

1.     Kuchunguza Tezi Dume kupitia njia ya haja kubwa au Digital Rectal Examination (DRE): Hiki ni kipimo cha kwanza kabisa ambacho mgonja hufanyiwa na daktari wake. Ni kipimo kinachoweza kumpa daktari picha ya tatizo na kufahamu kuhusu ukubwa na hali ya tezi dume. Daktari akiwa amevaa glovu huingiza kidole chake cha shahada katika njia ya haja kubwa au puru (rectum) ya mgonjwa kasha kuzungusha zungusha ili kufahamu kama tezi limevimba ama la na pia hali yake kama ni gumu kuliko kawaida ama lina utando na nyama laini.
2.     Kipimo cha damu cha Prostate-Specific Antigen (PSA): PSA husaidia kutofautisha kati ya saratani ya tezi dume na BPH. PSA ni aina ya protein inayozalishwa na seli za tezi dume na kiwango chake huongezeka iwapo kuna saratani ya tezi dume.
3.     Utrasound ya Puru (Rectal Ultrasound): Kipimo hiki hufanyika iwapo daktari atahisi kuwepo kwa saratani ya tezi dume badala ya BPH. Utrasound ya puru pamoja na kuonesha taswira ya tezi dume ilivyo, pia humuwezesha daktari kuchukua kinyama (biopsy) kwenye tezi dume kwa ajili ya uchunguzi zaidi ili kutofautisha kati ya saratani na BPH.
4.     Kiwango cha utokaji wa mkojo (Urine Flow Study): Ni kipimo kinachotumika kufahamu kasi ya utokaji wa mkojo. Mkojo unaotoka kwa kasi na kiwango kidogo huashiria kuwepo kwa BPH.
5.     Kipimo cha kuchunguza kibofu cha mkojo (Cystoscopy): Kipimo hiki husaidia kuweza kufahamu ukubwa wa tezi, sehemu tezi lilipobana njia ya mkojo na kiwango cha kubana huko. Aidha huwezesha pia kutambua hali ya kibofu cha mkojo ikoje.

Matibabu
Matibabu ya BPH yameganyika katika sehemu mbili, yale yanayofanywa kwa kutumia dawa na yale yanayofanywa kwa kutumia upasuaji mdogo. Aidha matibabu hufanywa kwa watu wenye BPH kubwa zaidi na dalili zinazowaletea usumbufu na kuathiri maisha yao, wakati wale wenye dalili ndogo ndogo hawalazimiki sana kuhitaji matibabu.
Matibabu kwa njia ya dawa
Dawa hizi hutumika kwa lengo la kulifanya tezi dume kusinyaa na kupungua ukubwa wake. Dawa hizo ni pamoja na

·   Finasteride na dutasteride ambazo huzuia uzalishajiwa homoni ya DHT. Matumizi ya dawa hizi husaidia kuzuia kukua na kuvimba kwa tezi dume au kulifanya tezi dume kusinyaa kabisa kwa baadhi ya wanaume.
·   Terazosin, doxazosin, tamsulosin na alfuzosin husaidia kulainisha misuli ya tezi dume na hivyo kupunguza mbano wa mrija wa urethra, hali inayosaidia mkojo kutoka vizuri.

Matibabu kwa njia ya asili
Kwa kuanza matibabu ya tezi dume mgonjwa aanze kwa kuepuka kula vyakula vigumu (all solid foods) na kunywa maji mengi ya kutosha kwa siku mbili hadi tatu. Maji yasiwekwe chochote isipikuwa juisi kidogo ya limao na yanywewe kula baada ya saa moja kupita. Hii husaidia utokaji wa mkojo kwenye kibofu cha mkojo. Baada ya hapo mgonjwa ale mlo wa matunda tu kwa siku tatu. Matunda hayo yajumuishe apples, pears, machungwa, mabalungi, zabibu, maembe, melons, na matunda mengine yenye maji maji. Mlo wa matunda husaidia kuondoa taka sumu (toxins) mwilini sanjari na kuondoa mafuta yaliyozidi katika mwili. Baada ya hapo mgonjwa ale mlo unaojumuisha milo miwili ya matunda na mlo mmoja wa mboga za majani kila siku kwa siku saba bila kula aina nyingine ya chakula. Mlo wa mboga za majani uliwe wakati wa jioni. Baada ya hapo mgonjwa ale mlo kamili (balanced diet) unaojumuisha nafaka (seeds, nuts and grains), mboga za majani na matunda. Tiba hii irudiwe baada ya kila miezi miwili au mitatu kutegemea ukubwa wa tatizo la tezi dume kwa mgonjwa.
Mbegu za maboga (pumpkin seeds) ni nzuri kwa kutibu tatizo la tezi dume. Tafuna mbegu hizi kila siku.

Matibabu kwa njia ya Upasuaji

Upasuaji mdogo (minimal Invasive procedures)

Upasuaji mdogo husaidia kuondoa dalili za BPH na hufanyika pale ambapo matibabu kwa njia ya dawa yameshindwa kuonesha mafanikio yeyote. Njia hizo ni:


·  Tiba ya kutumia mawimbi ya joto (Transurethral microwave procedures, TUMT): Tiba hii hutumia kifaa kinachotoa mawimbi ya joto (microwave) yanayochoma na kuharibu tishu zilizovimba za tezi dume. Matibabu huchukua chini ya saa moja na yanaweza kufanyika bila mgonjwa kuhitaji kulazwa.
· Tiba ya kutumia sindano maalum (Transurethral needle ablation, TUNA): Njia hii hutumia visindano vidogo ambavyo huunganiswa kwenye chombo chenye kutoa nishati ya joto kuunguza tishu zilizovimba za tezi dume.
· Tiba ya kutumia joto la maji (Water-induced thermotherapy): Tiba hii hutumia maji ya moto yaliyochemshwa kwa kifaa maalum kuunguza na kupunguza tishu zilizovimba za tezi dume.

Upasuaji mkubwa
Madaktari wengi hushauri kuondolewa kabisa kwa tezi dume iwapo itathibitika kuwa mgonjwa ana BPH. Zipo njia nyingi za upasuaji wa BPH, nazo ni pamoja na upasuaji kwa kupitia kwenye mrija wa mkojo (Transurethral surgery, TURP), upasuaji mkubwa wa wazi (Open surgery), upasuaji wa kutumia nishati kuondoa tishu za tezi dume (Laser surgery), na upasuaji wa kutumia joto la fibreoptic probe kuchoma tishu za tezi dume (Interstitial laser coagulation).

Vitu vya kufanya baada ya Upasuaji wa Tezi dume
Mara baada ya upasuaji wa tezi dume inashauriwa:
 
·    Kunywa maji kwa wingi ili kusafisha kibofu cha mkojo
·    Epuka kujikakamua sana unapojihisi kwenda haja kubwa
·    Kula lishe bora ili kuepuka kupata choo kigumu. Iwapo mgonjwa atapatwa na choo kigumu ni vyema amuone daktari ili amshauri jinsi ya kuondoa tatizo.
·    Epuka na acha kunyanyua vitu vizito.
·    Hairuhusiwi kuendesha gari wala kuendesha mtambo wowote ule mpaka utakapopona kabisa.

Matatizo yanayoweza kutokea baada ya upasuaji

· Shida wakati wa kukojoa: Kawaida huchukua muda wa siku kadhaa mtu kuweza kurejea katika hali yake ya kawaida ya kukojoa.
· Shida ya kuthibiti mkojo usitoke ovyo (Incontinence): Ni kawaida kwa mgonjwa kushindwa kuthibiti kutoka kwa mkojo katika siku za mwanzo baada ya operesheni. Hata hivyo hali hii hujirekebisha baada ya siku kadhaa kupita.
· Kutokwa na damu: Katika siku za wali mara baada ya TURP, kidonda kwenye tezi dume kinaweza kuvuja damu ambayo itaonekana katika mkojo. Hta hivyo hali hii hukoma baada ya wiki kadhaa. Hata hivyo iwapo utokaji damu ni mzito sana, inashauriwa kumuona daktari haraka.

Uwezo wa kufanya ngono baada ya upasuaji


Wagonjwa wengi waliofanyiwa upasuaji wa BPH uhofia sana kuhusu uwezo wao wa kufurahia tendo la ngono mara baada ya upasuaji. Kwa kawaida, huchukua muda fulani kwa agonjwa kuweza kurejea hali ya kawaida ya kufurahia tendo hili.


·  Mdiso au kudindisha (Erections): Madaktari wengi husema kuwa iwapo mgonjwa aliweza kupata mdiso au kudinda muda mfupi baada ya upasuaji, uwezo wake wa kuendelea kupa mdiso ni mkubwa zaidi. Hata hivyo iwapo mgonjwa hakuwa na uwezo wa kudisa tangu awali, upasuaji wa tezi dume hauna uwezo wa kumrejeshea uwezo wake wa kudisa.
· Kutoa mbegu (Ejaculation): Ingawa wanaume waliofanyiwa upasuaji wa tezi dume bado wanaweza kupata mdiso, mara nyingi upasuaji huu huwafanya wawe wagumba yaani wasioweza kupata watoto. Hali hii kwa kitaalamu huitwa retrograde ejaculation au kilele (mshindo) kikavu (dry climax). Kwa kawaida, wakati wa tendo la ngono, mbegu za kiume kutoka kwenye korodani huingia kwenye urethra karibu na kijitundu cha kibofu cha mkojo. Wakati wa tendo la ngono, misuli maalum hufunga kijitundu hicho ili kuzuia mbegu zisiingie kwenye kibofu badala yake zielekee kwenye urethra ya katika uume. Hata hivyo, upasuajiwa BPH huondoa misuli hiyo na kufanya mbegu kuingia kwenye kibofu cha mkojo badala ya kuendelea kwenye urethra ya uume. Shahawa hizo hatimaye hutolewa nje ya kibofu pamoja na mkojo.
· Kufika kilele (Orgasm): Huwa hakuna tofauti kubwa ya kufika kilele (orgasm) kabla na baada ya kufanyiwa upasuaji.

BPH na Saratani ya Tezi Dume: Hakuna Uhusiano wa moja kwa moja
Ingawa baadhi ya dalili za BPH zinafanan na zile za saratani ya tezi dume, kuwa na BPH hakuongezi uwezekano wa kupata saratani ya tezi dume. Hata hivyo, mwenye BPH anaweza pia na saratani ya tezi dume bila saratani hiyo kugundulika, ama wakati huo huo au siku za baadaye. Hivyo inashauriwa kuwa, ni vema wanaume wote kuanzia miaka 40 na keundelea kufanya uchunguzi wa tezi dume zao walau mara moja kila mwaka.
 

1 comment: